Na Hazard Mpango
Mwansaoka nguli duniani, Mbazil
Edson Arantes do Nascimento maarufu Pele alipata kunukuliwa akisema kuwa
mafanikio sio ajali bali ni utendajikazi wa nguvu, uvumilivu, kujifunza, na
kujitoa mhanga.
Kubwa zaidi ya yote hayo, Pele
aliyezaliwa Oktoba 23, 1940 na kuwika zaidi na timu yake ya taifa ya Brazili
‘Samba Boys’ miaka ya 1957 hadi 1971 alisisitiza kuwa ni kupenda unachofanya au
unachojifunza.
Ujumbe wa Pele nauona kama vile
haujabagua wa kuwafikishia. Ameutuma kwa walimwengu wote wanaotaka mafanikio
kwenye nyanja yoyote maishani mwao pasi na kujali ni kisiasa, kijamii au
kiuchumi.
Hata mashabiki wa soka nchini nao
wameguswa. Salamu za gwiji huyo wa kandanda duniani ziwafikie na wao pia,
lakini iwapo watakuwa wanataka mafanikio ya kweli kwenye mawanda ya soka.
Ni maneno ya hamasa kwao
yanayowasukuma mashabiki wa soka letu la bongo kujisaili iwapo malengo yao
yamefikia au la. Ni changamoto kubwa inayowapasa kutulia kuona namna bora ya kuitatua.
Mashabiki wenyewe wanajua na bila ya
shaka wanajifunza kutoka kwa wenzao wa nje ya mipaka ya nchi yetu na hasa wa
Uingereza. Wanawaona jinsi wenzao wanavyowachachafya makocha, wachezaji na
wenye hisa kwenye timu.
Wanawaona wenzao namna
wanavyopambana ili kusaidia mafanikio ya timu zao badala ya kulia, kupiga
kelele tupu uwanjani na kujipaka majivu usoni. Wenzao huko wanajitoa mhanga wa
kweli kiasi wanapozuiwa uwanjani timu inaathirika.
Kinyume na mashabiki wengi wa soka
la bongo ambao wao wapo nyuma na soka lenyewe. Hawawazi mafanikio ya kweli
zaidi ya kungoja ajali itakayowezesha soka la bongo lifanikiwe.
Hawataki kuumia kutokana na
kupigania soka iwe ni kufa au kupona. Wenyewe wamechoka kifikra, hawaoni mbali
kuhusu soka kwa ujumla ukiachana na mapenzi zaidi yaliyokolea ya timu kongwe za
Simba na Yanga.
Hawaamini kuhusu ubingwa wa nje ya
mipaka ya nchi kuanzia ngazi za vilabu na taifa. Miaka mingi vilabu vya nchi
yetu vimekuwa wasindikizaji kwenye mashindano makubwa barani Afrika, lakini
mashabiki hawajali.
Timu za taifa nazo zimekuwa ‘tia
maji tia maji’ miaka kibao, lakini mashabiki wamekuwa kimya kama sio wao vile.
Wanaacha soka likititia bila ya kelele ilhali nao wana nafasi ya kuliokoa.
Tatizo ni kuendekeza Simba na Yanga
kwa kiasi kikubwa na kusahau kuhusu soka. Vizazi vinarithishana kushabikia
zaidi timu hizi ambazo zimeishia kupokezana ubingwa wa ligi na mashindano ya
nyumbani na yale ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).
Hebu tazama mfano timu kongwe ya
Yanga ambayo imenzishwa tangu mwaka 1935 imeachwa nyuma na timu ya Asante
Kotoko ya nchini Ghana iliyoanzishwa mwaka huohuo ambayo imechukua ubingwa wa
Afrika mara mbili.
Imeshindwa na AS Vita Club ya
Kinshasa pamoja na CARA Brazzaville ya Jamhuri ya Kongo ambazo zimeanzishwa
mwaka mmoja na kupishana miezi, lakini timu hizo zimeshachukua ubingwa wa Shirikisho
la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) mara moja moja.
Pia Simba S.C iliyoanzishwa mwaka
1936 imeshindwa kusafisha nyota kama walivyofanya wenzao State d’Abidjan ya
nchini Ivory Coast ambayo imechukua ubingwa wa Afrika mara moja.
Ukiachana na timu zilizopata
mafanikio ingawaje zimeanzishwa mwaka mmoja na klabu zenye mashabiki wengi
nchini bado kuna timu nyingine zimeanzishwa miaka kadhaa baada ya timu zetu na
bado zimenyakua ubingwa wa Afrika.
Mfano wa timu ya ES Setif ya Algeria
imeanzishwa mwaka 1958 tayari imeshanyakua mara mbili, Enyimba F.C ya nchini
Nigeria imeanzishwa mwaka 1976 nayo imechukua mara mbili ubingwa huo wa klabu
barani Afrika.
Timu kamaWydad Casablanca ya Morocco
ilianzishwa mwaka 1937, Orlando Pirates F.C ya Afika Kusini, Asec Mimosas ya
nchini Ivory Coast zilianzishwa mwaka 1948, Union Douala ya nchini Cameroon na FAR
Rabat ya Morocco ailianzishwa 1958, zote zimechukua mara moja moja wakati klabu
ya Hafia F.C ya nchini Guinea iliyoanzishwa mwaka 1953 imechukua ubingwa wa
Afrika mara tatu.
Hebu mashabiki wetu wa soka waache
Usimba na Uyanga waangalie kuhusu soka kwa ujumla. Wasiishie kupiga kelele wajitoe
mhanga kwa kadiri ya uwezo wao ili yapatikane mafanikio kwenye soka ingawa
hatumlaumu dobi kutakasa kaniki.
0 maoni:
Chapisha Maoni
Click to see the code!
To insert emoticon you must added at least one space before the code.