Na Azard Mpango #UO 2
Kama vile ni mazingaombwe au uchawi kwa namna alivyokuwa
akifanya vitu vyake uwanjani. Alichezea mpira atakavyo, aliwapindua wapinzani
wake kwa kadiri alivyotaka na ilikuwa ni nadra mno mpira kupotea miguuni mwake.
Aliwapa wakati mgumu waliotaka kupambana naye kipindi akiwa na mpira miguuni
mwake kutokana na kuwa na chenga zenye maudhi zilizoacha uzito kwa mpinzani
aliyekuja kumkabili.
Alisifika kwa mbinu na maarifa ya hali ya juu awapo
uwanjani. Alitumainiwa kipindi chote kutokana na uhodari wa kubadili hali ya
mambo mchezoni na zaidi hakuwa mchoyo wa kutoa pasi. Mahali ambapo hakuna
anayetarajia kupita bado jamaa huyu aliweza na pengine hata kufunga. Baadhi ya
magoli yake amefunga akiwa chini ya ulinzi mkali wa wapinzani kiasi cha
kuwaduwaza wengi.
Ni kweli kuwa kila zama zina yake lakini tangu zama zake nahata
zinazoendelea bado anasakwa atakayelingana naye. Aliitwa ‘Mchawi wa Mpira wa
Miguu’ na akanadiwa kuwa ni mchezaji bora zaidi wa Nigeria ambaye hajapatapo
kutokea katika zama zake. Hakuwa na wa kumshindanisha kwa kipindi hicho na
baadhi ya wataalamu wa soka wanaamini hivyo mpaka sasa bado hajatokea Muafrika
wa aina yake.
Huyu ni Augustine Azuka Okocha aliyezaliwa Agosti 14, 1973
maeneo ya Enugu nchini Nigeria. Alikuwa akicheza nafasi ya kiungo mshambuliaji
na alipendelea mno kuvaa jezi namba 10 mgongoni. Kama wachezaji wengine hasa
kutoka bara la Afrika ambao historia zao za soka zinaanzia kwenye vilabu vya
mitaani, naye Okocha alianzia huko na kisha klabu ya Enugu Rangers iliyomtoa
golikipa maarufu nchini Nigeria, William Okpara.
Alizoeleka kwa jina la ‘Jay-Jay’ Okocha ambalo chimbuko lake
ni James Okocha kaka yake aliyeanza kucheza mpira wa miguu kabla ya Augustine
(mdogo mtu). James ndiye aliyekuwa amepewa jina la mitaani ‘Jay-Jay’ lililokuja
kuhamia kwa mdogo wake kiasi cha mwenye jina hilo kufunikwa na pengine mpaka
leo baadhi kutotambua asili ya jina hili.
Maisha matamu ya soka ya Okocha yalianzia nchini Ujerumani
alipokwenda kumtembela rafiki yake mmoja miaka ya 1990, ambaye alimshauri
kufanya majaribio katika klabu ya Borussia Neunkirchen iliyokuwa daraja la tatu
wakati huo na alifanikiwa kupata nafasi kutokana na soka safi alilokuwa
akilitandaza uwanjani.
Akiwa nchini Ujerumani mwaka 1992 alijiunga na klabu ya
Eintracht Frankfurt ambapo alikutana na mchezaji maarufu mwafrika kutoka nchini
Ghana, mshambuliajiu Tony Yeboah na baadaye akajumuika na mshambuliaji maarufu
Thomas Doll raia wa Ujerumani. Mwaka 1993 goli zuri alilomfunga mlinda mlango
Oliver Kahn lilichaguliwa na watazamaji wa kipindi cha michezo cha ‘ARD German
TV sports program’ kuwa goli la mwaka.
Mwaka 1995 Okocha alihama Eintracht Frankfurt na akabadili
upepo wa Ujerumani kwa kuelekea nchini Uturuki akajiunga na klabu ya
Fenerbahce. Katika msimu wake wa pili kwenye klabu yake nchini Uturuki, Okocha
alifunga magoli matatu ya ajabu ambayo hayataweza kusahaulika ndani ya klabu
yake. Akiwa nchini Uturuki humohumo Okocha alichukua uraia wa nchi hiyo na
kutumia jina la Muhammet Yavuz.
Maisha ya soka ya ‘Jay-Jay’ Okocha, mwaka 1998 yalihamia
nchini Ufaransa ambapo alijiunga na klabu ya Paris St-Germain (PSG) mahali
alipokutana na Mbazil Ronaldinho Gaucho. Hata hivyo katika majira ya joto mwaka
2002 baada ya Kombe la Dunia alijiunga na klabu ya Bolton Wanderers ya nchini
Uingereza.
Mashabiki wa Bolton walimpokea vyema na kumkubali huku msimu wake
uliofuata alipewa unahodha
ambapo aliiongoza klabu yake mwaka 2004 katika Kombe
la Ligi ambalo timu yake haikuwahiu kushiriki takribani miaka tisa.
Hata hivyo mwishoni mwa msimu wake klabuni Bolton alikwenda
Qatar kujiunga na klabu ya Qatar SC ambapo
baada ya msimu mmoja tu nchini Qatar, mwaka 2007 alirejea Uingereza na kujiunga
bure na klabu ya Hull City. Na kwa upande wa timu ya taifa ya Nigeria maarufu
kama Super Eagles, Okocha alianza kuonekana mwaka 1993 mpaka 2006.
Ajabu yake ni kwamba tangu aanze kucheza soka hakuwahi
kushinda tuzo ya mwanasoka bora Afrika hata mara moja kama walivyoshinda akina
Samuel Eto’o, Yaya Toure na wengine. Lakini bado Okocha aliwaambia mashabiki
wake kuwa analishukuru Shirikisho la Mpira wa Miguu barani Afrika (CAF) ambao
ndio waandaaji na watoaji wa tuzo hizo akisema kuwa ameweza kutambulika na
kupata tuzo nyingine.
Jambo kubwa na la msingi ni kwamba Okocha abakie kuwa darasa
kwa wachezaji wetu. Badala ya kuishia kusoma historia yake wajifunze na vitu
vyake alivyokuwa akifanya uwanjani. Okocha sio malaika aliyeshushwa toka
mbinguni hivyo basi hata wachezaji wetu wanaweza japo sio kufikia balaa zake
zilizompelekea kuitwa ‘Magic of Football’ lakini wakachota sehemu ya ufundi
wake kama alivyochota Ronaldinho Gaucho. Watanzania nao wajifunze kwake.
0 maoni:
Chapisha Maoni