Na Azard Mpango

Rais wa zamani wa Nigeria ambaye ni mwanajeshi mstaafu aliyeishia cheo cha Luteni Jenerali, Olesegun Mathew Obasanjo aliyezaliwa Machi 5, 1937 katika eneo la Abeokuta nchini Nigeria, ameamua kuongea kwa vitendo kuwa ameachana rasmi na siasa za Nigeria.

Obasanjo ambaye aliiongoza nchi yake kwa awamu mbili tofauti, awamu ya kwanza ilikuwa ni mwaka 1976 mpaka 197n akiwa Rais wa kijeshi aliyeteuliwa na Halmashauri ya Kijeshi na baadaye akaitisha uchaguzi wa kiraia ambapo Shehu Shagari alishinda na kuwa Rais mpya wa Nigeria.

Awamu ya pili ya Obasanjo ilikuwa ni mwaka 1999 mpaka 2007, ambapo alichaguliwa na wananchi kupitia chama cha People's Democratic Party (PDP). PDP ndicho chama tawala nchini Nigeria kinachoongozwa na Rais wa sasa Goodluck Jonathan anayegombea kwa awamu ya pili kwenye uchaguizi unaotarajiwa kufanyika mwezi Machi mwaka huu.

Mara nyingi mzee Obasanjo amelaumiwa kuwa hayuko pamoja na PDP, chama ambacho alikuwa kiongozi wa chama hicho katika cha urais wake wa awamu ya pili. Alinyooshewa vidole na ilifikia hatua kuonekana ni mpinzani hasa katika uongozi wa Rais Jonathan.

Rais Jonathan ni miongoni mwa waliomlaumu Obasanjo kwamba anakipigia debe chama kikuu cha upinzani cha All Progressive Congress (APC) kinachowakilishwa na Muhammadu Buhari hali inayomkatisha tamaa Rais Jonathan kwa sababu Rais mstaafu alitakiwa aokoe jahazi la PDP.

Obasanjo aliyejiunga na jeshi la Nigeria mwaka 1958 kama vile hakuwa na jibu la kuwapa wanaomlaumu kuunga mkono upinzani kwa sababu sauti yake iliwahi kusikika ikiahidi kuwa hatoweza kuachana na PDP na kama ikitokea basi hatajiunga na chama kingine.

Kwa kuwa Rais huyo mstaafu aliyepata kufungwa jela na kiongozi wa kijeshi Sani Abacha kati ya mwaka 1995 na 1998, hakueleweka vyema amerudia ahadi yake kuhusu PDP tena safari hii alikuwa akizungumza na viongozi wa chama hicho kutoka kata 11 waliomtembelea katika makazi yake ya Hilltop yaliyopo Abeokuta Kaskazini, nchini Nigeria.

"Niliwahi kuwaambia kuwa nilikuwa Rais kwa jukwaa la PDP, kwa heshima yake nikiondoka sitajiunga na chama kingine. Nitabakia Mnigeria wa kawaida, nipo tayari kufanyakazi na yeyote bila ya kujali itikadi yake ya kisiasa," Obasanjo aliwaambia wanachama hao.

Mzee Obasanjo hakuishia maneno hayo tu bali alitangaza rasmi kuachana na siasa na alichana kadi yake ya uanachama mbele ya viongozi wa PDP huku kabla ya kufanya jambo hilo gumu aliorodhesha mlolongo wa udhaifu wa Serikali ya Rais Jonathan.

Kwa kuchana kadi yake ya uanachama, tukio lililotokea katikati ya mwezi Februari mwaka huu, Obasanjo sio mwanachama wa PDP lakini alisisitiza kutojiunga na chama chochote. Kwa hatua hiyo bila shaka Rais huyo mstaafu ambaye alinusurika kuuawa na wapinzani nadi ya jeshi ni ishara kwamba amevunja ukimya na ameamua kujitenga na mikikimikiki ya siasa.


Hebu tujifikirishe kidogo! Mfano kitendo alichofanya mzee Obasanjo cha kuchana kadi ya chama, angekifanya 'Mzee wa Ruksa', Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi au 'Mr. Clean' Benjamin Mkapa, ingekuaje? Wananchi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wangesemaje?


Mkapa ambaye hakuonekana katika sherehe za makabidhiano ya Katiba Inayopendekezwa, imekuwa nongwa, vipi akichana kadi ya CCM? Leo analaumiwa na baadhi ya wananchi kwamba amejitenga mno na uongozi wa awamu ya nne, itakuwaje siku atakapotaja udhaifu wa Serikali iliyopo kama alivyojiamua Obasanjo? 'Kupumzika kama Obasanjo sio dhambi'   
22 Feb 2015

0 maoni:

Chapisha Maoni

:) :)) ;(( :-) =)) ;( ;-( :d :-d @-) :p :o :>) (o) [-( :-? (p) :-s (m) 8-) :-t :-b b-( :-# =p~ $-) (b) (f) x-) (k) (h) (c) cheer
Click to see the code!
To insert emoticon you must added at least one space before the code.

 
Top