Na Azard Mpango

Wachezaji wa Tanzania mpo? Mmemuona au kumsikia Mrisho Khalfani Ngasa anayechezea klabu kongwe ya Yanga iliyoanzishwa mwaka 1935 yenye makao makuu yake Jangwani? Mmemuelewa alichosema?

Ngasa ambaye pia ni mchezaji wa timu ya taifa ya Tanzania aliyezaliwa April 12, 1989 jijini Dar-es-Salaam, anayecheza nafasi ya ushambuliaji na kupendelea kuvaa jezi namba 17 alionekana kujilaumu waziwazi kwa kukataa kwake kujiunga na klabu ya Al-Merikh ya nchini Sudan kisa mapenzi yake kwa klabu ya Yanga. Ameeleweka?

Mshambuliaji huyo ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa klabu hiyo ya Yanga, alikataa mpango wa timu yake ya Azam iliyomsajili kwa gharama kubwa na timu ya Simba aliyokuwa akiitumikia kwa mkopo katika msimu wa 2012/2013 zilizotaka kumuuza Al-Mereikh.

"Nimekuwa nikikataa dili nyingi ninazopata kwa sababu ya mapenzi yangu ya Yanga," alisema Ngasa aliyewahi kuitumikia klabu ya Kagera Sugar msimu wa 2005/2006, Yanga 2006/2010 na baadaye Azam msimu wa 2010/2013 ambapo klabu ya Azam ilimpeleka klabu ya Simba kwa mkopo na kuitumikia msimu wa 2012/2013.

Ngasa aliyewahi kuwa mfungaji bora mwaka 2009 katika mashindano ya kombe la Kagame wakati akiitumikia timu ya taifa lake, kama vile ameipiga teke bahati katika soka ingawaje kwa umri wake lolote linaweza kutokea. Lakini kwa sasa Ngasa anajuta kubaki Yanga kisa anaipenda.
Mrisho Ngasa akitumikia Taifa Stars


"Leo ninajuta, nakumbuka nafasi hiyo niliyoipata kupitia Simba na Azam ndio ilikuwa bahati yangu ya kutoka kisoka," anasisitiza winga huyo aliyewahi kufanya majaribio mwaka 2009 katika klabu ya West Ham inayoshiriki ligi kuu ya Uingereza.

Pia baadaye mwaka 2011, Ngasa alibahatika kufanya majaribio mengine nchini Marekani katika klabu ya Seattle Sounders iliyowahi kucheza mechi ya kirafiki na klabu ya Manchester United ya Uingereza na Ngasa alicheza mechi hiyo akitokea benchi.

Leo winga huyo anasikitika ingawa anakiri hana wa kumlaumu zaidi ya nafsi yake. Wachezaji wanaojali zaidi ya mapenzi ya klabu zao na hatimaye kubaki hata ikitokea bahati ya 'mtende ya kuota jangwani', hebu wajifunze kwa mwenzao Ngasa.

Usijadili ubora wa Al-Mereikh dhidi ya Yanga kwa  sasa kutokana na ukweli kuwa mchezaji mwenyewe ameona kwenda huko kungemsaidia kutoka zaidi kisoka kuliko kubaki kwenye klabu anayosisitiza kuipenda.

Tujadili idadi ya wachezaji wanaokubali kusota benchi katika klabu zao kisa wanazipenda na kukataa kwenda klabu nyingine. Tujadili madhara kwa wachezaji hao ikiwemokuporomoka kwa viwango vyao na hasara inayoweza kuigharimu pengine mpaka timu ya taifa. Tujiulize kwamba wachezaji hawa wanajielewa kweli?

Ni lazima kuwa wawazi kwamba mchezaji kupenda timu yoyote sio mwiko wala dhambi na ndio maana tunamuona nahodha wa klabu ya Liverpool, Seven Gerrard aliyezaliwa Mei 30, 1980 pale Whiston, Merseyside nchini Uingereza namna anavyoipenda klabu yake iliyomlea tanghu mwaka 1987 na bado anaitumikia.

Ni vigumu kumlinganisha Ngasa na Gerrard kwenye upande wa mapenzi ya klabu zao kutokana na jambo moja tu kwamba Gerrard hakupata kujuta kubaki katika klabu anayoipenda ya pale Anfield kama Ngasa alivyoijutia klabu anayoipenda ya pale Jangwani. Hapa kuna masafa!
Winga machachari wa Yanga, Mrisho Ngasa, akimtoka beki wa Ruvu Shooting, Stepano Mwasika, wakati wa mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom.

Sasa ni muda wa wachezaji wetu wa 'kibongo' kufungua macho ya kufikiri ili waweze kumuona Wayne Mark Rooney aliyezaliwa Oktoba 24, 1985 pale Croxteth, Liverpool nchini Uingereza. Rooney alilelewa katika klabu ya Everton tangu mwaka 1996 na anauthibitishia ulimwengu kuwa hakuna klabu anayoipenda na kuishabikia zaidi ya Everton.

Nani hajui kama Rooney anaitumikia Manchester United? Nani atashindwa kujibu swali kwamba kwanini Rooney ameiacha klabu anayoipenda inayotumia uwanja wa Goodison Park na kuhamia kwa 'Mashetani Wekundu' wanaotumia uwanja wa pale Old Trafford? Na lini tumemsikia Rooney ameujutia uamuzi.

Ngasa ametoa somo la bure kwa wachezaji wetu karibu wote hapa nchini hivyo wajifunze. Wakumbuke kwamba kama mapenzi pekee ya timu yanatosha kumbakiza mchezaji hata kama atasota benchi basi angebaki Raul Gonzalez Blanco pale Santiago Bernabeu.


Raul aliyezaliwa Juni 27, 1977 pale San Cristobal de Los Angeles nchini Hispania, aliipenda klabu ya Real Madrid (Los Blancos), timu iliyomlea tangu mwaka 1992 na mpaka akapewa heshima kuwa 'alama ya timu,' lakini baada ya miaka 16 ndani ya Real Madri alitimkia Shalke 04 ya nchini Ujerumani. Wachezaji wajifunze! 


22 Feb 2015

0 maoni:

Chapisha Maoni

:) :)) ;(( :-) =)) ;( ;-( :d :-d @-) :p :o :>) (o) [-( :-? (p) :-s (m) 8-) :-t :-b b-( :-# =p~ $-) (b) (f) x-) (k) (h) (c) cheer
Click to see the code!
To insert emoticon you must added at least one space before the code.

 
Top