Siku za hivi karibuni kumeripotiwa
kupatikana kwa mkanda wa video unamuonesha mtu aliyevalia mavazi meusi (kama
ninja) na miwani ya giza aliyejiambulisha kuwa anaitwa Kais bin Abdullah, na
kuthibitisha kushiriki katika uvamizi wa baadhi ya vituo vya polisi, kupora
silaha, kuua na kujeruhi askari polisi.
Kwa mujibu wa taarifa hizo ni kwamba
bin Abdullah alidai kushiriki kufanya vitendo hivyo viovu na vya kikatili kwa
ajili ya kulipa kisasi cha siku nyingi. Anadai kuwa wenzao saba kutoka mkoa
Mtwara wamekamatwa kwa makosa ya dhulma, kupanga na ugaidi.
Anawataja wenzake wengine 21 kwamba
wamekamatwa huko Zanzibar na wamepelekwa gereza la Segerea jijini
Dar-es-Salaam, 18 kutoka Mwanza wamepelekwa gereza la Kisongo, Arusha na
wengine 19 wameuawa kabisa huko mkoani Mtwara.
Bin Abdullah anadai kuwa subira yao
imefika kikomo na walichokuwa wakisubiri Mungu ameshawapa na badala yake
kupitia video hiyo inayoonekana kulisakama jeshi la polisi nchini wametoa ahadi
kwa kusema:"...kilichopo hivi sasa tunatoboa jahazi wote tuzame."
Ahadi hiyo na nyingine zilizokuwemo
ndani ya video hiyo ni taa nyekundu ya tahadhari kwa jeshi la polisi, serikali
pamoja na vyombo vyake vya usalama kuwa makini na utayari kwa lolote lile.
IGP Mangu akisisitizajambo
Lisipuuze na kuyaona ni mambo ya
kisiasa au ni uongo na uzushi mkubwa na badala yake liamke na kuanza
kufuatilia. Lijipange kwa mapambano, lijilinde na kuwalinda wananchi ambao
hawana hata elimu au mbinu yoyote ya kukwepana na mashambulizi kama haya na
pengine hawajawahi kukutana nayo.
Kujihadhari kabla ya hatari ni vyema
kuliko kuingoja. Raia wanaliangalia jeshi la polisi ambalo bin Abdullah
ameliandama huku akikumbushia uvamizi wa baadhi ya vituo vya polisi, kupora
silaha, kuua na kujeruhi askari polisi.
Niseme tu kwamba hata kama video ya
bin Abdullah ni ya vitisho au ina malengo mengine, bado jeshi hilo lisipuuze na
kujiona lipo salama au hakuna atakayeweza kuwadhuru raia ambao jeshi la polisi
lina dhamana ya kuwahakikishia usalama wao pamoja na mali zao.
Madhila dhini ya jeshi la polisi
yalikuwepo na bado yanaendelea hivyo jambo la msingi ni kujipanga kwa jeshi
hilo. Mathalani ni mara nyingi vituo vya polisi vinavamiwa na wananchi
wanaoitwa wenye hasira kali na kuvishambulia vituo hivyo na hata pengine kuleta
uharibu katika vituo hivyo.
Pia siku za hivi karibuni, jeshi
letu la polisi limezidi kuandamwa. Ukiacha kuvamiwa kwa askari wake kipindi
wakiwa kwenye maeneo yao ya kazi akama ilivyowatokea askari wenye namba G369PC
Mansour na HV507PC Mwalimu, wakiwa doria ya pikipiki walinyang'anywa silaha
zenye namba 14301230 na 143035 bado vituo vyao navyo vinavamiwa na kufanyika
uporaji na pengine mauaji.
Mfano, Juni 2014, moja ya kituo
kidogo cha polisi huko mkoani Pwani kilivamiwa na watu wenye silaha za jadi,
walimjeruhi vibaya askari mwenye namba D9889 Koplo Joseph Ngonyani aliyekufa
wakati akitibiwa hospitali ya wilaya, Mkuranga na askari Mariamu Mkamba
alijeruhiwa (amepona baada ya matibabu), lakini wavamizi walipora silaha.
Septemba 2014, kituo kikubwa cha
polisi cha Ushirombo kilichopo wilaya Bukombe, mkoa Geita kilivamiwa na katika
uvamizi huo wameuawa askari polisi wenye namba WP7106Pc Uria Mwandiga na
G2615PC Dustan Kimati, wakati askari polisi wenye namba E5831CPL David Ngupama
na H627PC Mohamed Hassan walijeruhiwa na wavamizi walipora silaha.
Januari 2015, kituo cha polisi
Ikwiriri, wilaya Rufiji mkoani Pwani kilivamiwa na kuuawa askari polisi wawili
wenye namba E8732 Koplo Edga Mlinga (askari wa kikosi cha usalama barabarani)
na WP5558 Judith Timoth na wavamizi walipora silaha wakati mapema mwezi Februari
mwaka huu, kituo cha polisi Mngeta, wilaya Kilombero mkoani Morogoro kilivamiwa
na kuibiwa baadhi ya vitu ikiwemo silaha yenye risasi zaidi ya 20, kutoka na
msako wa polisi vitu hivyo vilipatikana na baadhi ya watuhumiwa wamekamatwa.
Kwa matukio haya na mengine
yanayoliandama jeshi letu la polisi, bila shaka ni kengele ya kuamsha umakini
wa jeshi hilo kuanzia kwenye vituo vyao ambavyo 'bin Abdullah' anajisifu kuwa
wameweza kuchukua silaha hali wenyewe (wavamizi) hawakuwa na silaha. Umakini
huo pia unapaswa uwe kwa nchi nzima kutoka na ukweli kuwa macho ya wananchi
yanawatazama.
Video ya 'bin Abdallah'
ilisahaulishe jeshi ile hadithi yao ya visu vya Chama cha Wananchi-CUF na
nyingine zinazonasibishwa kisiasa zaidi. Jeshi la polisi liamke na kufuatilia
kwa umakini wa hali ya juu uhalifu unaotamalaki kiasi inafikia raia
kulinyooshea kidole jeshi hilo kuwa limeshindwa si tu kuwalinda wananchi bali
hata kujilinda.
Wananchi nao wasikubali kuunga mkono
aina yoyote ya uhalifu na kinyume chake washirikiane bega kwa bega na jeshi la
polisi ili kutokomeza vikundi vinavyoweza kuingiza nchi yetu katika mabalaa
kama yale ya Al-Shabab ya Somalia na Boko Haram ya huko Nigeria.
Jeshi la polisi nalo liumize kichwa
usiku na mchana ili kupata mbinu ya kuwanasa wavamizi wa vituo vyao na
ikiwezekana kurejesha mikononi mwao silaha zilizoporwa au kuibwa kwa sababu
zitatumika kufanyia uhalifu mwingine ikiwemo kulipia kisasi cha siku nyingi
kama alivyosema 'bin Abdullah' kwenye mkanda wa video ulioripotiwa kuwepo hasa
Dar-es-Salaam.
Tunakiri kuwa tumepata hasara
isiyolipika kwa kuwapoteza ndugu, jamaa, rafiki na wasimamizi wetu pamoja na
mali zetu, hivyo naliomba jeshi la polisi lisipuuze kipenga cha hatari ya
ugaidi kilichopulizwa na Kaisi bin Abdullah.
ni kweli jeshi letu linapaswa kuwa makini kwa suala hilo pia sisi wananchi tushirikiane na vyombo vyetu vya usalama hili ni tatizo
JibuFuta