Na Azard Mpango #UO 2


Karibu nchi zote barani Afrika zinatumia katiba kama muongozo na sheria mama. Katiba ndicho kitabu kitakatifu katika nchi ambacho hufuatwa na raia wote na kuheshimiwa. Kutii katiba ni lazima si tu kwa watawaliwa bali hata kwa watawala wa ngazi za chini na juu.

Ni mwiko kuifanyia kitendo chochote cha kuonesha kuidharau katiba ya nchi na kufanya hivyo ni kosa ambalo huenda likapelekea kuchukuliwa hatua kali za kisheria. Pia kuvunja katiba ni kwenda kinyume na sheria kwa yeyote yule awaye.

Mfano nchini Tanzania aliyekuwa mwasisi na Mwenyekiti wa chama cha Tanzania Labour Party (TLP) daktari wa mifugo Leo Lwekamwa aliwahi kuikanyaga katiba ya nchi mwishoni mwa mwaka 1997 katika viwanja vya Jangwani. 

Nyendo za baadhi ya viongozi wa juu katika nchi za Afrika kama vile zinaanza kutisha. Hatua nzito wanazopiga huku wakiangalia pembeni zinatoa ishara mbaya ya kutaka kuonesha dharau ya kukanyaga katiba ambazo wenyewe ndio wasimamizi wakuu.

Polepole wanakaribia kuzisigina lakini kwa sauti ya ukali kabisa wenyewe wanadai wanafanya marekebisho, ambapo ajabu yenyewe marekebesho yanataka kufanyika wakati wakiona viatu walivyovaa wanapaswa kuvua. Haviwatoshi wamekua.

Kama vile hawasikii sauti za waliokuwa pembeni wakiwatazama na kuwakumbusha kuwa hatua wanazopiga ni kukimbilia kukanyaga kitabu kitakatifu kinachofuatwa na watu wa dini mchanganyiko, hadhi na rangi tofauti.

Wanataka kukanyaga makusudi kwa sababu vilivyomo ndani yake havina urafiki nao. Badala ya kukaribishwa wanaagwa hali wameshanogewa au hofu ya kuwa peku baada ya kutembea kwa muda mrefu tena kwa kishindo kikubwa ardhini huku wametinga viatu vya bei mbaya.

Maneno mfano wa haya yaliyokuwemo katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, toleo lake la 2005 ibara ya 40 (2) yasemayo: “Hakuna mtu atakayechaguliwa zaidi ya mara mbili kushika kiti cha Rais.” Hawayapendi na ndio hayo yanapelekea kunadi marekebisho mapema.

Rais wa Rwanda na kiongozi wa chama cha Rwandan Patriotic Front (RPF), Paul Kagame aliyezaliwa Oktoba 23, 1957 huko Tambwe, Ruanda-Urundi (Nyarutovo ya sasa), anatarajiwa kumaliza muhula wake wa pili mwaka 2017 na katiba ya Rwanda haimpi ruhusa ya kuongoza kwa muhula mwingine.

Wakati Rais Kagame akiwa kimya, vyama vitatu vya upinzani kikiwemo PDI cha Waziri wa Mambo ya Ndani, Musa Fazil Hererimana, PSP na tawi la chama cha PS-Imbarakuri vimeonesha kumhitaji Rais Kagame aendelee kuongoza.

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)  Joseph Kabila aliyeingia madarakani baada ya kuuawa na wanajeshi baba yake Laurent Desiree Kabila mwaka 2001, amekusudia kufanya mabadiliko kipengele namba 220 cha katiba ili ikiwezekana aweze kushiriki uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwaka 2016.

Kabila aliyezaliwa Juni 4, 1971 katika mji wa Hewa Bora mkoa Kivu na alipata kusoma katika mikoa ya Dar-es-Slaam na Mbeya huku akisemekana kutumia jina la Hippolyte Kanambe Kazemberembe Kabange Mtwale kwa sababu za kiusalama anamalizia muhula wake wa pili na tayari baadhi ya wapinzani wameshaanza kupinga harakati hizo. Katiba yao ni mihula miwili.

Rais wa Uganda Yoweri Museveni na Rais wa Zimbabwe  Robert Mugabe

Msemaji wa Ikulu ya Bujumbura, Willy Nyamitwe amethibisha kuwa Rais Pierre Nkurunziza aliyezaliwa Disemba 18, 1963 anatarajia kugombea kwa muhula wa tatu iwapo chama chake ambacho yeye ndiye Mwenyekiti cha National Council for the Defense of Democracy Forces for the Defense of Democracy (CNDD-FDD) kitamchagua.

Huko Oagadougou, Burkinafaso sauti za wananchi wanaozuia wakubwa wasikanyage katiba kwa ajili ya kuendelea kuishi Ikulu, zimemuondoa kabisa mwaka 2014 Rais wa tangu mwaka 1987, Kapteni Braise Compaore’ aliyezaliwa Februari 3, 1951 ambaye alikuwa kiongozi wa chama cha Congress for Democracy an Progress (CDP) na yuko uhamishoni nchini Morocco.

Rais  Abdoulaye Wade wa Senegal aliyepewa ruhusa ya kuongoza mihula mitatu na Mahakama ya Katiba huku wananchi wakipinga kitendo hicho cha Rais kuwa kimevunja katiba, alikubali kushindwa na mpinzani wake Macky Sall. Wananchi walimkataa kwa wingi Wade aliyekanyaga katiba.

Mzee ‘Jongwe’ wa Zimbabwe, Robert Gabriel Mugabe aliyezaliwa 21 Februari 1924 aliyeingia Ikulu  tangu 1987 bado yuko madarakani kwa zaidi ya miaka 20 na katiba iliyopitishwa miaka ya usoni imeweka ukomo wa miaka mitano kwa muhula mmoja.

Rais wa Guinea ya Ikweta ambaye ni mwanajeshi wa zamani Teodoro Obiang Nguema aliyezaliwa Juni 6, 1942 maeneo ya Acoacan, Spanish Guinea aliyempindua mjomba wake Fransico Macias Nguema, mwaka 1979 hajaonesha nia kama anahitaji kugombea tena urais na inasemakana mwanaye anatazamiwa kurithi iwapo Rais huyo ataachia madaraka hayo.

Rais Yoweri Kaguta Museveni aliyezaliwa Agosti 15,1944 maeneo ya Ntungamo, Uganda amekuwa Rais wa Uganda tangu 1986. Museven aliyewahi kusoma Chuo Kikuu cha Dare-es-Salaam na kiongozi wa chama cha National Resistance Movement (NRM) aliitisha uchaguzi wa vyama vingi wa kwanza mwaka 2006 na aliushinda upinzani.


Itoshe kusema kwamba katiba zilizotungwa na wawakilishi wa wananchi ziheshimiwe ili kulinda machafuko yanayopelekea kupoteza roho za makumi kwa mamia ya wananchi. Inatosha yaliyotokea Libya, Misri na Tunisia kuwa funzo kwa viongozi wakuu wa nchi za Afrika kuheshimu katiba na kuachia madaraka pale inapobidi.

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top