Na Azard Mpango                     
           
Siku ya hafla fupi ya kuagwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Tanzania na wa pili kwa Tanganyika mzee Rashid Mfaume Kawawa (maarufu Simba wa Vita) alipokuwa anastaafu rasmi siasa za majukwaani aliahidi kufa akiwa mwanachama muaminifu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kawawa miongoni mwa waasisi wa CCM alizaliwa Februari 26, 1926 katika kijiji cha Matepwende, wilaya Songea mkoani Ruvuma alikufa mwezi Disemba mwaka 2009, aliyasema hayo mbele ya swahiba wake Mwalimu Julias Kambarage Nyerere.

Mwalimu Nyerere ambaye ndiye Mwenyekiti wa kwanza wa CCM, chama kilichotokana na muungano wa vyama viwili ambavyo ni Tanganyika National Union (TANU) cha Tanganyika na Afro Shirazi Party (ASP) cha Zanzibar, alipopata nafasi katika hafla hiyo alimjibu Kawawa.

Nyerere aliyezaliwa tarehe 13 mwezi Aprili katika kijiji cha Butiama mkoani Mara, ambaye kitaaluma ni mwalimu alikufa tarehe 14, Oktoba 1999 huko London, Uingereza katika hospitali ya Mtakatifu Thomas alikopelekwa akisumbuliwa na kansa ya damu.
Mwalimu Kambarage Nyerere

 Aliongoza Tanganyika kama Waziri Kiongozi katika utawa wa kikoloni (1960-1961), Waziri Mkuu wa Tanganyika (1961-1964), Rais wa Tanganyika (1962-1964) na baadaye Rais wa Tanzania mpaka alipoamua kuachia madaraka kwa hiyari Novemba 5, 1985.

Mwalimu Nyerere aliyesimamia kuungana kwa TANU alichokuwa akikiongoza na ASP kilichokuwa chini ya hayati Sheikh Abeid Amani Karume, katika hafla hiyo alimwambia Kawawa kwamba ana roho ngumu kwa kuahidi kuifia CCM.

“ Rashid una roho ngumu, utakufa mwanachama muaminifu wa CCM? Mimi siwezi kuyasema hayo, CCM inaweza kubadilika. Siku ikiacha misingi nami naachana nayo, kwa sababu si mama yangu,” aliyasema Mwalimu mbele ya mzee Kawawa aliyeahidi kufa katika uaminifu na CCM.

Leo Simba wa Vita aliyeahidi kuifia CCM hayupo, Mwalimu aliyeikana CCM kama ikiacha misingi yake naye pia hayupo lakini matukio pamoja na nukuu zao zitabaki kama vielelezo kwa wafuasi wa vyama vya siasa hasa CCM ili waweze kujifunza.

Wajiulize ni kwanini muasisi na Mwenyekiti wa kwanza wa chama kikongwe nchini aliwahi kukikana chama chake? Wafuatilie kwa kina hiyo misingi yenyewe ya CCM kwamba bado inafuatwa ili hata kama Mwalimu Nyerere angekuwa hai aendelee kuwa mwana-CCM.

Hakuna tatizo kwa Rashid kwa sababu aliahidi kufa ndani ya CCM hata kama kikipoteza dira lakini alama ya kiulizo ibaki kwa Mwalimu ambaye ni mfuasi mtiifu wa itikadi ya Kijamaa na Kujitegemea kuwa angeendelea kuwa mwana-CCM mpaka sasa? CCM hii bado inalinda misingi yake kweli?.

Moja ya misingi ya CCM ni kwamba Ujamaa na Kujitegemea ndiyo njia pekee ya kujenga jamii ya watu waliosawa na huru. Hata Mwalimu Nyerere analisisitiza hili la usawa kwenye chapisho lake la Ujamaa la mwaka 1962. Je msingi huu bado upo CCM hii inayoadhimisha kuzaliwa kwake kila ifikapo Februari 5?.

Tarehe 5, Februari 1967 Mwalimu alianzisha Azimio la Arusha ikiwa ni msisitizo wa vitendo katika kutekeleza itikadi ya Ujamaa lakini mwaka 1992, Halmashauri Kuu ya CCM ilipitisha azimio la Zanzibar ambalo lilionekana kufungua milango ya utegemezi kwa kukubali matakwa ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa.

Kupitia azimio hilo CCM ilikubali sera ya vyama vingi, ilipokea ubinafsishaji uliokaribisha wawekezaji na kuruhusu soko huria na utegemezi. Azimio la Zanzibar kama vile liliua rasmi lile la Arusha ambalo lilizaliwa tarehe na mwezi unaofanana na wa CCM lakini limefifilizwa.

 Tunakumbushwa kuwa miongoni mwa misingi ya CCM ni kwamba binadamu wote ni sawa. CCM hii inakiri hilo? Leo tunauzungumzia usawa upi wakati kuna masafa marefu baina ya watawala na watawaliwa, masikini na matajiri? Mwana-CCM yupi anakumbuka kutekeleza msingi huu wa usawa?.


Misingi ya CCM ilianza kupindishwa tangu uhai wa muasisi wake na inaelekea kufukiwa kiasi cha kuwafanya baadhi ya makada waanze kukitofautisha chama hicho, mfano aliyewahi kushika wadhifa wa Uwaziri Mkuu na Mwanasheria Mkuu wa nchi mzee Joseph Sinde Warioba alisema yeye ni mwanachama hai wa CCM lakini sio CCM ‘maslahi’. Mwalimu aliikana CCM ipi sasa?

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top