Na Azard Mpango #UO 2
Siku za hivi karibuni
katika mkoa wa Tanga kumezuka taharuki kiasi cha kutikisa hali ya amani na
utulivu nchini. Vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na baadhi ya watu
wamekuwa wakitoa taarifa wanazozijua kuhusiana na tukio hilo..
Wapo waliodai kwamba
kilichokuwa kikiendelea huko Tanga ni mapambano baina ya jeshi la polisi
lililoomba msaada Jeshi la Wananchi la Tanzania (JWTZ) na magaidi tena
wakiwataja kuwa ni Al Shabbab toka Somalia.
Kuna waliokuwa wakitoa
idadi isiyothibitishwa ya majeruhi na vifo na wengine hasa kwenye mitandao ya
kijamii wakijaribu kuweka picha ambazo si za tukio halisi kiasi cha kuwapa hofu
wananchi zaidi wasiokuwepo eneo la tukio.
Baadhi ya waliopata
fursa ya kutumia kalamu walihamisha tukio hilo ambalo lilitawaliwa na piga
nikupige ya silaha za moto kuwa ni la kisiasa. Wanaamini kuwa ni mchezo
unaofanywa kisiasa ili kuondoa fikra za wananchi katika mambo yanayowakabili
kama vile kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa, kujiandikisha katika daftari
la wapiga kura na mengine.
Imefika wakati baadhi
ya wananchi wanasema bila ya kuwa na uhakika wowote tena mbele ya watu wengine
kuwa ni kazi ya Serikali. Yaani Serikali imetengeneza makusudi tukio la Tanga
pasipo kuwahurumia wananchi wake.
Hii ni hatari ambayo si
tu inaweza kuwachonganisha wananchi kuichukia Serikali yao bali inawezekana
kuwa chachu ya kuanzishwa kwa vikundi vya uasi nchini. Lengo la wanaojaribu
kuingiza hisia na chuki binafsi katika matukio mazito kama haya ya Tanga ni
kujipalia makaa ya moto.
Wakati tukisherehekea
maendeleo ya kisayansi na teknolojia ni lazima tuzijue athari zake hasi na
chanya. Teknolojia imetusogeza karibu na kuwa mithili ya kijiji kimoja lakini
inatupa nafasi ya kufungua fikra zetu ili zihariri yaliyosogezwa na maendeleo
hayo.
Inatupa muda mwingine
zaidi ya kutegemea wahariri wa magazeti,redio na televisheni kupitia na kuchuja
kilicholetwa na maendeleo hayo yanayoonekana kukua kwa kasi. Mitandao ya
kijamii si tu imeturahisishia kupata habari bali inatupa changamoto ya
kuzithibitisha habari hizo.
Tunajua fika kuwa Jeshi
la Polisi ndilo lenye kuweza kuthibitisha kuhusu mwenendo wa tukio hilo la
Tanga ambalo bado linaendelea kusisitiza kuwa sio la kigaidi, hao wanaoandika kuwa
ni Al Shabab wanatoa wapi na wana agenda gani? Na picha zisizohusiana na tukio
zinatumika kwanini?
Taarifa zinazonasibisha
Serikali au chama tawala kuwa nyuma ya mpango huu wa tukio la Tanga
zimethibitishwa na nani? Kama ni kutumia mazowea tu inatosha kujikumbusha
matukio ya uhalifu yaliyofanyika miaka ya nyuma kuwa nayo yalifanywa kwa baraka
za Serikali au chama?
Wananchi tuamke kifikra
sasa badala ya kutegemea uongo unaotungwa na baadhi ya watu huenda wasiolitakia
mema taifa letu au kutokujua walitendalo. Kuna video mbalimbali zinasambazwa
ili kuoanisha matukio ya kihalifu nchini, zisipuuzwe na kinyume chake bongo
zipewe muda wa kuchunguza ukweli wake.
Tukio la Tanga
linatosha kuwaamsha vijana ambao kwa asilimia kubwa ndio wahanga wa mchezo huu
mchafu na watumiaji wakubwa wa mitandao ya kijamii, kutokukurupuka na kuunga
mkono harakati zisizoieleweka kichwa wala miguu.
0 maoni:
Chapisha Maoni