Na Azard Mpango #UO 2                   
Bila shaka tumesikia kwamba matokeo ya mtihani wa kidato cha nne uliofanyika mwaka jana (2014) yametangazwa na kiwango cha ufaulu kwa mujibu wa Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), Dk. Charles Msonde kinaonekana kuongezeka kuliko mwaka juzi (2013).

Dk. Msonde alisema kuwa jumla ya  watahiniwa 196,805 ambao ni sawa na asilimia 68.33 (68.33%) ya watahiniwa wote walifaulu mtihani wa kidato cha nne ikiwa ni ongezeko la asilimia 10.08 (10.08%) ukilinganisha na mwaka 2013 ambapo wanafunzi 235,227 sawa na asilimia 58.25 (58.25%) ndio waliofaulu mtihani.

Kumbukumbu zinaonesha kuwa mwaka 2012 waliofaulu ni asilimia 43, mwaka 2011 asilimia 53.6, mwaka 2010 asilimia 50.4, mwaka 2009 asilimia 72.5, mwaka 2008 asilimia 83.6, mwaka 2007 asilimia 90.6, 2006 asilimia 89.12, na mwaka 2005 ni asilimia 89.3. Kifupi sikumbuki kama kuna mwaka walifaulu asilimia mia moja kuanzia elimu ya msingi mpaka sekondari.

Binafsi nawapongeza waliofaulu mitihani ya kidato cha nne lakini nawakumbusha kuwa bado wanapaswa kuomba Mungu zaidi kwa sababu kuna kigingi mbele yao cha kubahatika kuchaguliwa kujiunga na kidato  cha tano. Wapo wanaochaguliwa na wapo pia wanaoachwa.

Kuchaguliwa kujiunga kidato cha tano kwa wale waliofaulu mitihani ya kidato cha nne na kuchaguliwa kujiunga na elimu ya juu kwa wale waliofaulu mitihani ya kidato cha sita ni shughuli nyingine pevu. Si ajabu kuchaguliwa lisilo chaguo la mwanafunzi (muombaji).    

Hatua hii inamfananisha mwanafunzi na mfungwa kwa jambo moja kwamba mfungwa hachagui gereza badala yake ni bahati tu kupangiwa gereza alilokuwa akifikiri kupelekwa kama ilivyo mwanafunzi anayewaza na pengine kuchagua shule au chuo, mchepuo au kozi na hatimaye kutopelekwa huko apendapo.

Wapo wanafunzi wengi ambao wamepangiwa wasichochagua na mfano mzuri ni ndugu yangu wa damu ambaye alichagua michepuo ya Sayansi akachaguliwa kusoma kidato cha tano na sita masomo ya Sanaa (Arts) na Chuo Kikuu alichagua kozi ya ‘Business Administration’ badala yake akachaguliwa kujiunga kozi ya Elimu.

 Hata kama kuna vigezo wanavyoviangalia wachaguaji lakini ukweli unabaki kuwa tatizo kubwa wachaguaji hawana taarifa za wanaowachagua. Hawajui hao wanaowachagua wanapendelea kozi au michepuo ipi na kwanini?.

Kuchagua wanaotoka darasa la saba kwenda sekondari kwa mfumo wetu wa elimu hakuhitaji kuwaumiza wachaguaji kumfikiria wanayemchagua kwamba anapenda mchepuo gani kwa sababu huko wanakwenda kuchanganya masomo yote labda kidato cha tatu ambapo pia  ni juu ya walimu kujadiliana na wanafunzi kwa kuangalia uwezo wa masomo ya darasani.

Kinyume na anayechaguliwa  kujiunga kidato cha tano, kwanza anakwenda kusoma baadhi ya masomo kama ni Historia, Jiografia na Lugha ya Kiingereza (HGL) ni hayo tu na anayeomba kuchaguliwa bila shaka amejiaminisha kuwa amefanya vizuri masomo anayoomba kuchaguliwa na hivyohivyo kwa waombaji wa elimu ya juu wanaomba kile wanachokimudu.
Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi Shukuru Kawambwa


Kitendo cha anayeomba mfano masomo ya Fizikia, Kemia na Hesabu (PCM) halafu po akachaguliwa kusoma masomo ya Uchumi, Jiografia na Hesabu (EGM) ni kumuharibia mapendekezo yake, lakini kwa kuwa ni mfungwa hana namna zaidi ya kutumikia kifungo hicho.

Wale wa kidato cha sita ambao mfano wanaomba kozi ya Sheria halafu wanachaguliwa kozi ya Elimu, bila shaka kutakuwa na msuguano japo wa ndani ambapo kuna watakaosoma kwa shingo upande, hali hii inaweza kupelekea kutokuwa na wataalamu waliopenda taaluma zao tangu awali.


Kwa maana hii huenda tusilalamikie utendaji mbovu wa wataalamu wetu kwa sababu inawezekana taaluma walizosomea walilazimishwa na mfumo wa elimu au wachaguaji. Kuna kuna kazi kubwa ya kuchagua wanafunzi waliofaulu kutokana na kile wanachokipenda ingawaje wapo ambao wanatumikia kile walichoomba na kuchaguliwa. Wahitimu waombe Mungu waangukie kwenye machaguo yao.

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top