Na Hosea Mchopa

Macho yao ni meupe kama wanamatumaini na siku ya kesho,kucha zao fupi ukiwauliza watakujibu ni watu wa amani hatupo tayari kushambulia.Mimi siko tayari kuwasubiria waamke nitawaamsha kwa wimbo wa taifa.

Usimwache mwizi aingie ndani kwako  mara tatu.Mara ya kwanza ilitosha,mara ya pili ilikuwa ni nafasi.Mara ya tatu ina maana wewe ni mjinga.Tumewapa jina jipya wanunuzi wa mboga tukiwasifu kwa ujanja huku tayari wameshatuibia.

Mawazo yakiwa mengi katika kichwa chako ujue una mambo unatakiwa uyafanye.Ajabu wao ni wepesi kusoma na kucheka ama kulalamika kisho kukunja gazeti na kuondoka.

Wana jina jipya siku hizi ‘Wadanganyika’,hulikubali na kucheka kuwa limebuniwa tu kutokana na jina la Tanganyika.Hakuna tafsri mbaya kama ya kuhisi jibu lisilo na mashiko ukalipa asilimia 100.

Tumeharibika ubongo tunaweka imani kwa mtu kutokana na hela zake na wenye ubongo ulioshiba tunawaita wapiga kelele.Tumebadilika sana kama hatujawahi kuwaza juu ya kizazi kijacho.Watukoseao tunawasifu kuwa wana macho ya makengeza.

Bado wana imani kuwa nchi jirani zinakuwa kwa kasi kutokana na udogo wa nchi wala si uhodari wao.Hii upelekea kuamini sisi lazima tukue taratibu kwa kuwa nchi yetu ni kubwa yenye mikoa 26.Uvivu siku zoye huongozwa na mbinu za ulegevu.

Buddha aliona mbali na kusema “fikra ni kila kitu,kile unachofikira ndivyo utakavyokuwa”.Tunawaza bado kuwa wale ndio wanainama kwa masaa kutunga sheria nchi itaendaje.Wale wakiinuka ndio wataendesha nchi watakavyo na sisi tutazame na kumuinamia anayekubaliwa na wao.

Baadhi ya wachungaji wamakanisa nao wanaelemewa na misaada ya ujenzi wamakanisa.Wanakubali kuta zilizosimama zije miaka mitano kuwagharimu kuirudisha Tanzania waliyoizoea.Je watahubiri kwa kujikosoa na kulia machozi ya damu kuonesha kujutia.

Baadhi ya viongozi wa kiislamu ‘masheikh’ nao wanalazimika kuwatumikia watu hatari ambao watawafanya waumini wao wasiifaidi nchi yao miaka ijayo.Heri tunyamaze kimya mana ukimya unalipa.Siku zote ukimya wa wananchi ni onyo kwa kiongozi.

Kama tumeshindwa kukwepa kwa nini tusiwe wanafiki kwao tunazidisha ukaribu usio na tija katika hadhi ya wadhifa wetu katika jamii.Tutembee na ule msemo kuwa sisi ni watu wakutanguliza  wenzetu mbele.Tena hatari ikiwa mbele.

Wataalamu wetu wamekuwa watumwa maarufu wameamua kuharibu hata mfumo wa matumaini kwao.Sasa ni ngumu kuwatofautisha wao na wale waliokosa bahati ya elimu.Wamebakiwa na maneno ya jeuri kuwa wanafahamu nchi nyingi kutokana na umaarufu wao.

Bado hatuna nia ya kuamini uongozi ni nafasi maalumu iliyopangwa kwa ajili ya kuwatumikia watu.Bado tunaamini kiongozi ni yule aliye na uwezo mkubwa wa kifedha katika jamii anayewaza kutimiza majukumu yetu kutoka mfukoni kwake.

Mungu ibariki nchi yangu Tanzania.Maana watanzania wenyewe hawafahamu hakuna Tanzania bila watanzania.Bado hawana nia ya kuamua kulinda ardhi kwa ajili ya vitukuu vyao.


0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top