Na Azard Mpango

Wataalamu ni watu muhimu katika jamii. Nchi yoyote duniani inahitaji kuwa na wataalamu wa fani mbalimbali ili kuweza kupata maendeleo kuanzia ya kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyotolewa na Taasisi ya Uchung uzi wa Kiswahili (TUKI) toleo la tatu imetoa maana ya neno mtaalamu ambalo wingi wake ni wataalamu kuwa ni mtu mwenye elimu, ustadi au ujuzi wa fani au jambo Fulani maalum. Na hata Tanzania watu hao wapo.

Kazi ya wataalamu ni kutumikia kile walichosomea au walichokuwa na ujuzi nacho. Mfano mtaalamu wa masuala ya uchumi aoneshe umwamba wake katika uchumi, wa siasa na siasa na elimu naye kwenye elimu. Kifupi ni kwamba kila mtaalamu anapaswa  atumikie utaalamu wake.

Kwa maana hiyo tulitarajia taifa letu ambalo lina wataalamu wengi mno wa fani mbalimbali lingepiga hatua. Wataalamu wetu wangesaidia kwa kiwango kikubwa kama sio chote nchi yetu kutononoka.

Lakini kama vile siasa ya nchi yetu imewakataza wataalamu kutumikia utaalamu wao na badala yake inawafunga kamba na kuwaburuza waingie kwenye kwenye jengo la maamuzi ya kisiasa mahali ambapo utaalamu sio kigezo kikubwa cha kupewa kiti cha heshima.

Nao pasipo kujali hilo wameamua kutundika vyeti vyao na kuacha kutumikia kwa wasaa mpana utaalamu wao na kuamua kukimbilia katika siasa.

Wataalamu hawajifungii ndani au kuzuunguka huku na kule kwa ajili ya kufanya tafiti mbalimbali bali wanachofikiria ni namna ya kuwa wabunge, madiwani na pengine Rais, basi.

Siasa imewateka wataalamu wetu wengi ijapokuwa sio wote kama vile wa afya, sheria, elimu, uchumi na wengine wa fani tofauti. Wengi wao hawatumikii tena utaalamu wao bali wanatumikia siasa ambayo kuwashushia heshima zao si kazi ngumu kwasababu haijali utaalamu.

Huenda ni kwa sababu mfumo wa siasa uliopo unaonekana kusita kumtazama mtaalamu kinyume chake unamtaza zaidi mwanasiasa. Marupurupu, mishahara minono na pengina hata posho nzuri anazopata mtaalamu ni tofauti na mwanasiasa ambaye huenda hana hata utaalamu wa siasa anayoitumikia.

Kivutio kikubwa cha maslahi kilichopo kwenye siasa kimekuwa ni chambo wa kuwapata wataalamu wetu kukimbilia huko pasipokujali kudhalilika. Heshima na hadhi zao zinagaragazwa hadharani kiasi cha kuwatia aibu, lakini wenyewe hawajali kitu.

Wataalamu wameamua kuipigia magoti siasa badala ya kutumikia utaalamu wao ambao ungeweza kuibadili siasa yenyewe. Wataalamu wetu ambao kimsingi ni kundi muhimu katika jamii wametumbukia kwenye dimbwi lenye tope linalotoa harufu mbaya kiasi cha kuwatukanisha mbele ya jamii.


Utaalamu wao sio heshima tena kwa jamii na ndio maana mpaka vinywa vya wasioweza kuwafikia vimethubutu kuwaita majina yasiyopendeza na yanayoonesha kutojali utaalamu wao. Aibu wanayopata inachafua na hata kutia walakini utaalamu wao. ‘Eeee! Mola waopoe wataalamu wetu.’

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top