Na Azard Mpango

Nimekumbuka maneno ya wahenga wetu waliposema kwamba ukila na kipofu usimshike mkono. Nimeyakumbuka haya huku ikiwa imepita miaka takribani saba tangu tushikwe mkono tukiwa kwenye sahani ya umasikini, lakini ni siku chache tena hali hiyo imejirudia. Tumeshikwa tena.

Katikati ya mlo mwaka 2008 kipindi tukijua tupo masikini peke yetu kwenye nyumba ya Tanzania, ghafla tukashikwa mkono na msomi Andrew John Chenge tena alijisahau akasema kwa sauti kuwa zile dola milioni 40 za rada kwake si chochote ni ‘vijisenti’ tu. Aliwaambia waandishi wa habari kwenye uwanja wa ndege wa Mwalimu J.K. Nyerere alipowasili akitoa nchini China.

Rada hiyo ilinunuliwa katika kipindi cha Rais Benjamin Mkapa (sasa mstaafu) wakati Chenge aliyepata shahada yake ya pili ya sheria (Master of Laws) katika chuo cha Harvard cha nchini Marekani, moja ya chuo bora duniani alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Andrew Chenge


Waliomuona walimfuatilia mpaka wakagundua kuwa alikuwa na akaunti nje ya nchi iliyokuwa na zaidi ya dola milioni moja. Kelele za waliostuka zilipenya kiasi kwamba zilimpelekea Chenge kujiuzulu nafasi ya Waziri wa Miundombinu aliyoteuliwa na Rais Jakaya Kikwete mwaka 2006.

Wengine kwa upofu wetu tukadhaniwa hatujui na ndio maana hata akateuliwa kuwa Waziri wa kwanza wa Afrika Mashariki (2006) na baadaye Waziri wa Miundombinu (2006-2008). Kisa ni kule kukubali kumchagua mwaka 2005 kuliwakilisha jimbo la Bariadi Magharibi huku akijulikana fika kuwa amevamia sahani wasioweza kuita dola milioni 40 ni vijisenti.

Katika hali ileile ya kujisahau kuwa wanakula na nani, mwezi Februari 2015 mbunge wa Muleba Kusini Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka alisema kuwa alitoa mapema kiasi cha shilingi milioni 10 kwa ajili ya kununulia mboga. Alisema hayo kipindi akijitetea alipokuwa akihojiwa na mwanasheria Getruda Cyriacus wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kuhusu sakata la fedha za akaunti ya Tegeta Escrow.
Anna Tibaijuka


 Bado wanaamini vipofu wanaokula nao hawana uwezo wa kuhisi hata wakiguswa na ndio maana wanafanya watakavyo. Wanachojua watawakaribisha tu (kuwachagua) kwa kuwa hawakuwaona wala kuwahisi kama nao waliokuwepo kwenye sinia ileile ya awali. Roho nzuri ya vipofu (wananchi wanaowachagua) inawapa kiburi wenye macho (viongozi).

Mengi yamepita ikiwemo falsafa ya ANGUKA (yaani Ari,Nguvu na Kasi) na hayakuonekana na ndio maana panakuwepo na nguvu inayoshawishi kauli za ajabu. Wananchi wanalia kila uchwao kutokana na kutoona faida ya kukua kwa pato la taifa, kushindikana kuwakabili kikweli maadui wa Tanzania aliowataja baba wa taifa na bado kimya kinatawala.     

Ifike wakati viongozi wetu wajue kwamba wanawaongoza watu wengi wasiokuwa na uwezo sio tu wa kuziona dola milioni 40 ni vijisenti au kutumia milioni 10 kwa ajili ya mboga bali hiyo milo mitatu kwa siku ni shida, hivyo wachunge wanachokisema hata kama ni kweli. Viongozi wawe waogopa wa kutoa maneno pasipo kuyapima mara mbili kwa sababu yanaweza kuinua hasira za wananchi wanaowatarajia wawapigie kura katika chaguzi mbalimbali.


N.B: sikutumia neno vipofu kwa ajili ya kuonesha dharau ya kundi hili bali nimelazimika kutumia kutokana na methali niliyoanza nayo, samahani kwa yeyote aliyekwazika na hilo.

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top