Na Azard Mpango

Mwandishi wa vitabu ambaye pia ni Mhadhiri mzaliwa wa Missouri katika jimbo la Florida nchini Marekani, Samuel Langhome Clemense aliyekuwa akipendelea kuitwa Mark Twain alipata kusema kwamba hofu ya kifo hutokana na hofu ya kuishi.

Mark Twain mwandishi wa kitabu kitwacho “Adventures of Hucklebery Finn (cha mwaka 1885) ” aliyezaliwa Novemba 30, 1835 na kufa Aprili 21, 1910 huko Redding, Connecticut nchini Marekani katika nukuu yake alisisitiza kwamba mtu aliyehai hujiandaa kwa kifo kitakachomfika muda wowote.

Maneno haya yenye nguvu katika bongo za wenye kufikiri yalinigusa pale nilipopata taarifa ya kifo cha aliyekuwa Mbunge wa jimbo la Mbinga Magharibi kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kapteni (mstaafu) John Damiano Komba ambaye alikufa akiwa njiani wakati akipelekwa hospitali ya TMJ ya jijini Dr-es-Salaam.

Taarifa za awali kuhusu kifo cha mbunge huyo ambaye pia aliwahi kuwa Mkurugenzi wa kikundi cha sanaa cha Tanzania One Theatre (TOT) na mwimbaji maarufu nchini nilizipata kupitia mitandao ya kijamii hasa ‘Facebook’ na ‘WhatsApp’ ingawaje zilionesha vyanzo vya taarifa hizo ikiwemo Redio Uhuru inayomilikiwa na CCM.

Sikushtushwa na taarifa za kifo cha Kapteni Komba kwa kuwa niliamini kwamba kwa mwanadamu kufa si kiroja kama anavyojihakikishia mcharaza gitaa Johnny Allen Hendrix (Jimi Hendrix) aliyezaliwa Novemba 27, 1942 pale Seattle, Washington nchini Marekani kuwa yeye ni miongoni mwa watakaokufa pale muda utakapotimu. Hata Kapteni Komba ni miongoni mwao!

Nilishangazwa na namna wapokeaji walivyotoa maono (comments) yao ambayo mengi niliyoyaona yalikosa huruma na simanzi ya kiutu na kinyume chake yalijaa kebehi, chuki zilizojengwa kisiasa na laana kwa Kapteni Komba. Yalikuwapo maneno makali kiasi cha mengine kumhukumu kabisa hata kabla ya kuwekwa kwenye makazi mapya (kaburini).

Hata salamu za kumtakia mapumziko mema (Rest In Peace) za wengi wao zilikuwa na shida kwa sababu ziliandikwa kimazowea na sio kuagizwa na nyoyo za huruma zinazomsukuma mwanadamu kuguswa na kifo cha kiumbe mwenzake anayemithilika naye. Hesabu za haraka zilitoa majibu kwamba ‘R.I.P’ nyingi kama sio zote zilikuwa za wana-CCM na waliozowea ama kujisikia uvivu kutoa ‘comments’ zao.

Lengo si kumsafisha Kapteni Komba aliyeishi zaidi ya miaka 50 ulimwenguni tena kwenye gurudumu lenye mikimiki la siasa kama za Tanzania bali kukitazama kifo chake kama shule kwa waliobaki. Natambua fika kwamba mahali alimopita marehemu enzi ya uhai wake kuna mambo mabaya au pengine ya kuudhi aliyatenda ama kuyasema lakini kurasa zake zimefungwa na hakuna wa mwanadamu wa kuzisahihisha tena halafu akamrejeshea.

Hayo yanabaki kuwa ni majeraha kwa walioguswa na zaidi katika maisha ya mwanadamu aliyeishi umri kama wa Kapteni Komba na hata pengine wa chini yake hawezi kusalimika na madonda ya lawama kwa sababu si kila alifanyalo maishani mwake wanajamii watalipokea kwa mikono miwili na ukarimu.
Hivyo mwanasiasa huyu ameondoka na makovu yake kama vile anavyojiapiza mwandishi wa riwaya na nyimbo, Charles Michael Palahniuk (Chuck Palahniuk) aliyezaliwa eneo liitwalo Pasco pale Washington pindi aliposema kuwa hawezi kufa bila ya makovu. Na vivyo hivyo ndivyo alivyokufa Mjumbe wa Kamati Kuu (NEC) ya CCM.
Marehemu John Komba

Funzo kubwa kutokana na vifo  vya wanadamu kikiwemo cha Kapteni Komba ni kujisahihisha na kujitathmini badala ya kuwalaumu waliokufa. Uhai si wasaa wa kuanza kuhesabu mema na maovu ya marehemu bali ni nafasi adhimu ya kupanga namna ya kuiacha dunia. Si nafasi ya ‘kupost’, ‘kuchat’ au kupoteza muda kwa waliohai bali ni kipindi cha maandalizi ya kifo, hivyo kunahitajika kujipanga kwa sababu utaacha majeraha.

Kapteni Komba aliyezaliwa Machi 18, 1954 na kufa jioni ya Februari 18, 2015 alipata kusema kuwa mwanadamu anapaswa kujua kuwa kufa kupo ingawaje si vyema kukifikiria lakini mchekeshaji na mwandishi, Allan Stewart (Woody Allen) aliyezaliwa Disemba 1, 1935 alipata kusema kuwa haogopi kufa bali hataki kuwepo pale (kifo) kinapotokea.


Tuliokuwa hai sasa ni wafu wa baadaye, tujitahidi kutumia vyema fursa ya uhai wetu kwa sababu hata Kapteni Komba hakujua kama ni 2015 ndio kifo chake huenda angejisahihisha na kuomba msamaha kwa aliyowakosea. Kifo chake ni hofu kwetu.

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top