Na. Hosea Mchopa
Wewe ni nani katika jamii yako na unaipa nini jamii yako
inayokuzunguka.Na wala sio wewe umepata nini katika jamii na una nini katika
jamii.Fikra ni kila kitu katika siku ya kesho lakini kuwaza hakuwezi kukupa
picha ya kesho utashiriki nini.Ni fumbo la karne lenye ukurasa zisizoisha kuzichambua.
Wakati mgumu siku zote hutengeneza jambo jema na la kuvutia
katika maisha ya binadamu.Kujitafakari huibuka sehemu pekee ambayo Mungu
naamini anatamani kila mwanadamu aipate hii nafasi.Hutufanya kuwa tulioshuka
tukitazama juu na kuamini kuna kitu tunahitaji kurekebisha.
Maya Angelou aliwahi kusema nimejifunza watu watasahau
ulichosema,watu watasahau ulichotenda,lakini hawatasahau jinsi ulivyowafanya wahisi.Kuna
wakati tutasahau walichofanya wakiwa wametangulia mbele za haki.Lakini watu
wanaweza wakahisi nini moyoni wakisikia jina lako.
Kujitafakari kwa kina huzaa matunda yaliyo na gharama kubwa
sana katika maisha ya binadamu.Matunda haya hugharimu muda,maumivu,tamaa mpya
na maamuzi ya kishujaa.Kujitafakari huja baada ya makosa,huja baada ya kupotea
njia,huja baada ya kuhisi hatutapita panapostahili.
Ni rahisi sana kupata nafasi hii ya muhimu ambayo inaweza
kuweka alama moyoni mwako.Alama ambayo itakufurahisha baada ya kurekebisha au
itakuumiza kwa kujua bado unaendelea kukosea.Bahati iliyoje kujitafakari
kunaweza kukatokea kupitia wengine.
Nasikia huzuni iliyo kubwa napoona binadamu wanachochea kuni
moto huunguzao nyumba ya jirani.Ilihali wao hawana mkataba na siku
inayokuja,kinachoumiza hawajapata nafasi muhimu ya kujitafakari.Hakuna ajuayesiku
ya kesho kwa aliyekosa na aliyekamili.
Jamii inaweza ikawa na tafsiri nyingi mbaya juu ya mwanadamu Fulani.Lakini
anayeamini fikra ni mali huendana kinyume na tafsiri zao pekee hutaka kutumia
ile nafasi kuamini wao pia hawajakamilika.Wao hutumia fursa ile kujionya kuwa
sipaswi kujiona bora kwenye kila kitu napaswa kuwa na macho yenye kunionyesha
hatari mara nyingi iwezekanavyo.
Sauti ya gharama siku zote haifungamani upande wowote
husimama katikati ya pande nne za dunia na kutuliza upepo wa kus na kas.Kwa
nini tusitumie makosa waliofanya wenzetu kujitafakari na kuamua kesho ipi
idondokee machoni petu.
Kesho yetu nani anaidhamini kwa kuhukumu,kulikoni kusahihisha
ili wasiopata muda wa kujitafakari wasafiri nasi.Walikosea wametangulia hatuko
nao tena katika ulimwengu huu ambao wametokea.Lazima tuongee kuhusu wao kwa
sababu walikuwa watu wakubwa katika jamii yetu lakini tunaitumia nafasi hii
vyema kutengeneza kesho yetu.
Rafiki yangu alikuwa mlevi wa kupindukia na alisifika kila
kona alipopita.Katika maisha yake ya nyuma alidharau walevi kulikoni watu
wowote wafanyao maovu katika jamii.Yeye hakutumia nafasi kutafakari siku zake
za usoni juu ya sababu zipelekeazo ulevi.Wala hakuwahi kujitafakari nyendo zake
zipo njia gani.
Alipofika chuoni akajichanganya na mwishoe akaangukia katika
ulevi uliopindukia.Akawa kiumbe cha ajabu hajui alichofuata chuoni wala jamii
yake inahitaji msaada gani kutoka kwake.Baadaye akapata mkasa uliomfanya
atafakari juu ya ulevi,unampa nini na unamfanya awe nani katika jamii.
Akanipa funzo kubwa sana kipindi cha nyuma hakutumia nafasi
ya athari za walevi wengine kujitafakari yeye.Yeye aliishia kuwadharau na
kuwalaumu kitu ambacho akikumweka karibu na Mungu ili aweze kupanda matunda
yenye gharama.Leo hii ameitumia nafasi vyema ya kujitafakari kwa na ameachana
na ulevi.
Na amepata nguvu ya kuweza kukomboa waliothika na ulevi.Walikuwa
viongozi wakubwa na waliishi katika jamii yetu kinyume na matarajio yetu.Lakini
tunaangalia mgawanyo wa muda wetu katika kunung’unika kwa waliyotenda na
kujitafakai upya kwa njia walizopita.
Maisha yana mwisho tena usiojulikana kwa kila mmoja,hatupaswi
kutumia muda mwingi kulaumu visivyo jibu.Tutumie ule muda kujitafakari na
kuonyesha njia ya kupita ili wakati wako ukifika watu wajae na hisia za
ulivyowafanya waone kuna kitu cha pekee ndani ya moyo wako.
0 maoni:
Chapisha Maoni