Na Leonard Kadago #UO 3
                                      
Katika maisha ya kawaida kuna binadamu ambao tangu wamekufa hakuna aliyezaliwa kuziba mapengo yao. Hali hiyo inatokana na uwezo mkubwa wa kufanya  ambo mbalimbali pamoja na busara walizojaliwa na Mungu.

Miongoni mwa watu hao ni mwanamapinduzi Thomas Isidore Sankara aliyezaliwa Disemba 21, 1949 maeneo ya Yako, French Western African (Burkina Faso ya sasa) aliyeuawa Oktoba 15, 1987 Orgadou, Burkina Faso.

Sankara mwanajeshi aliyefikia cheo cha Kapteni aliyepata kuwa Rais wa Burkina Faso kati ya 1983 na 1987 aliwagusa wengi kiasi kwamba wananchi wa Burkina Faso wamefikia kukiri kuwa hakuna Rais aliyefanana naye au kumkaribia kutokana na uzalendo pamoja na uaminifu aliokuwa nao kwenye rasilimali za taifa hilo lililopo Magharibi mwa Afrika.

Mifano ya watu kama Sankara ipo mingi mno katika maisha yetu ya kila siku kuanzia kwenye ngazi ya familia, kata, wilaya, mkoa na taifa kwa ujumla wake. Kuna watu wengi hasa viongozi ambao wamefanya mambo mengi mazuri ambayo hakuna binadamu aliyewakaribia.

Watu hao si tu wapo kwenye masuala ya siasa peke yake bali  mpaka kwenye michezo. Wapo hadi kwenye soka letu la nyumbani  na mpaka kwenye Ligi Kuu yetu ya Vodacom. Wapo mpaka kwenye klabu zetu  za bongo ikiwemo na kikosi cha Simba maaarufu kama Wekundu wa Msimbazi.   
Marehemu Patric Mafisango

Kumbukumbu chungu kwa Wana Msimbazi ni ile iliyotokea Mei 17, 2012 ambapo walimpoteza kiungo mkabaji aliyekuwa na uwezo wa hali ya juu wa kutumia guu lake la kushoto kila anapokuwepo uwanjani. Huyo ni Patrick Mutesa Mafisango aliyezaliwa Machi 9, 1980 pale Kinshasa, Zaire aliyekufa njiani wakati akikimbizwa hospitali baada ya kupata ajali ya gari jijini Dar es Salaam.

 Hakuna shabiki wa Simba na pengine hata wa klabu nyingine ambaye atalisahau jina la Mafisango aliyekuwa na asili ya Kongo ambaye alichukua uraia wa Rwanda. Jamaa alikuwa anaujua na alifanya kazi yake kwa ustadi wa hali ya juu na ndio maana aligeuka na kuwa kipenzi cha mashabiki wa soka na hasa wa klabu ya Simba.

Kifo cha Mafisango kimeacha pengo kubwa kwa wana Msimbazi na wapenda soka nchini. Kimewaacha wengi midomo wazi lakini furaha kwa klabu ya Simba imeanza kurejea baada ya kumpata kiungo ambaye uwezo wake unafanana na ule wa Mafisango. Kiungo huyo anatumia mguu kama wa Mafisango.

Kwa wale waliobahatika kutazama au kufuatilia mechi za hivi karibuni ilizocheza klabu ya Simba na Coastal Union pamoja na ile iliyowakutanisha na Polisi Morogoro bila shaka watakuwa wamemuona mchezaji aliyevaa jezi namba 24 mgongoni.

 Ni Abdi Banda ambaye alisajiliwa kama beki akitokea klabu ya Coastal Union lakini ujio wa kocha kutoka Serbia Goran Kopunovic umekuwa kama neema inayowakumbusha mbali wana Msimbazi kwa sababu kocha huyo amembadili namba kutoka kucheza nafasi ya beki mpaka kiungo mkabaji.
Kiungo wa Simba Abdi Banda


Kila mpenda soka anapata furaha moyoni kumtazama kiungo huyu kutokana na ukweli kuwa huwa anafanya kazi yake kwa kujituma na kila pasi anayotoa inafika palipostahili na ni mara chache kupoteza mpira. Banda ana umbo la kimpira na hasa urefu wake unamfanya kugeuka burudani wa kila anapogusa  mpira.

Iwapo mchezaji huyu  wa klabu ya Simba atajifunza na kutolewa sifa  bila shaka ataisaidia klabu yake pamoja na timu ya taifa kutokana na ukweli kwamba  umri wake unaruhusu. Shughuli yake awapo uwanjani inawafunika viungo wengi wa nyumbani.

Yote tisa, kumi ni kile kiwango alichokionesha katika pambano la Watani wa Jadi (Simba na Yanga)lililofanyika  Machi 8, mwaka huu kwenye uwanja wa taifa lililoishia kwa Simba kushinda goli moja lililowekwa kimiani na Emanuel Okwi.

Banda alifunika safu ya kiungo ya watani wao iliyokuwa ikiongozwa na Haruna Niyonzima. Alikaba kwa nguvu na alitandaza pasi zenye macho muda wote wa mchezo huo. Uwepo wa Banda na kiwango anachokionesha akiwa na uzi wa Simba kinakumbusha uwepo wa Mafisango mwingine.

Miaka ya  hivi karibuni klabu ya Simba imezalisha wachezaji wengi vijana  kama vile Jonas Mkude, Saidi Ndemla, Abdallah Seseme, Ramadhani Singano, Ibrahim  Ajibu, Haruna Chanongo pamoja na nahodha wa timu hiyo Hasani Isihaka lakini ujio wa kijana Banda anayetumia mguu wa shoto kama Mafisango  ni faraja kwa wana Simba na wapenda soka safi. ‘Bravo Abdi Banda’ lakini usilewe sifa.


18 Mar 2015

0 maoni:

Chapisha Maoni

 
Top