Na Azard Mpango
Muigizaji ambaye pia ni mchekeshaji, Roseanne Charrie Barr
aliyezaliwa Novemba 3, 1952 huko Salt Lake City nchini Marekani alipata kutoa
somo kwa wanawake wenzake kwamba jambo moja wanalotakiwa kujifunza ni kuwa hakuna
yeyote atakayewapa nguvu (power), hivyo wanatakiwa wachukue.
Bila shaka aliyasema hayo kutokana na historia ya kuteseka
na kutengwa kwa wanawake ulimwenguni. Atakuwa ameyakumbuka machungu waliyopata
wanawake wenzao na pengine kuna maeneo mpaka sasa bado wanaendelea kuyapata
ingawaje ni tofauti na zama zilizopita.
Amekumbuka namna mwanamke alivyochukuliwa kuwa ni chombo cha
starehe pekee na sio vinginevyo. Mwanamke hakuonekana ni kiumbe bora mbele ya
mfumo kandamizi unaohisiwa kwamba mpaka leo bado haujafutika na umeendelea
kukita mizizi yake tena mpaka katika fikra za binadamu wa karne ya sayansi na
teknolojia.
Kwamba bado mawazo mgando ya kumdhania mwanamke kuwa ni
mshindwa yangalipo ijapokuwa sura ya mwanamke mwenyewe inaonekana karibu kila
mahali. Si katika majeshi, uongozi mbalimbali, michezo, viwandani, biashara na
maeneo mengine mengi tu mwanamke naye yupo. Leo mpaka kumimina zege nao
wanajichanganya.
Kule kulikoitwa kupigania haki za wanawake kunaonekana
kupatikana kwa matunda yake ingawaje si kwa kiwango kikubwa. Vita ya kuwatetea
wanawake haipaswi kukoma kwa sababu ya kuonekana kwamba wameanza kupumua kwa
kushirikishwa karibu katika kila mahali kuanzia ofisini mpaka nyumbani.
Sauti kali ya utetezi isishuke na badala yake ipazwe ili
iende zaidi ya hapa ilipo sasa. Anayenadi asiogope kukauka koo kwa sababu birika
lililojaa maji yenye baraka linakuja. Kila nchi kwa nafasi yake isichoke kuwapa
nguvu wanawake ikiwa ni pamoja na kutunga kanuni na sheria zitakazotilia uzito
suala hilo na sio kuwabeba.
Ni lazima ieleweke kuwa wanawake hawapaswi kupewa upendeleo
wa aina yoyote bali wapewe nguvu na ndio maana hata mwanamama Roseanne
amewakumbusha hilo. Kumpa mwanamke upendeleo si kumuinua wala kumtoa kwenye
mfumo dume unaopigwa vita bali ni kumlemaza na kumuhakikishia kwamba ni kiumbe
dhaifu anayengoja kubebwa kwa kila kitu.
Lakini kama vile wanawake wenyewe nao hawalioni hili au
wanaogopa kukataa. Ule unyonge wao uliokuwepo tangu zama na zama unaendelea kwa
aina tofauti kidogo siku hizi. Enzi zile walinyongeshwa pasipo kutarajia
kinyume na enzi hizi ambazo kwa mikono yao miwili wanapokea aina zote za
unyonge tena kwa furaha.
Ukimya wa wanawake wengi wa Tanzania dhidi ya kaulimbiu
zenye ukakasi kwao ni ishara kwamba wameanza kusahau kama wenzao walipitia kwenye
njia zenye miiba kabla ya kufika hapa ilipo leo. Wenzao waliosimama kidete
kutetea haki za wanawake hawakutaka upendeleo wa aina yoyote zaidi ya nguvu.
Wanaambiwa eti wakiwezeshwa wanaweza! Wao
wanarukaruka kwa mapambio. Kwanini wasihoji kuwezeshwa huko? Mbona wanasahau
kwamba waliambiwa wachukue na sio kusubiri kuwezeshwa kama wanavyofanya siku
hizi?
Wanasubiri kupewa ubunge wa viti maalum. Wanasubiri alama za
chini za wastani wa kufauluhuko mashuleni na wanasubiri huruma na upendeleo
karibu kila mahali. Huku ni kurudishwa nyuma tena wakati wapambanaji
walishaanzisha na kilchobaki ni muendelezo wa kuchukua na sio kupendelewa.
Wanawake wa Tanzania wanaendelea kutengeneza unyonge
usiomithilika iwapo wataendelea kupokea nafasi za upendeleo badala ya kuchukua
nafasi zao. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 si
inasisitiza kuwa kila binadanu huzaliwa akiwa huru na sawa, sasa ni kwanini
wanawake washindwe mpaka wawezeshwe?
Leo tunaelekea katika uchaguzi mkuu lakini kutokana na
kujisahau kama wanawake ni sehemu ya binadamu huru na sawa kama walivyokuwa
wanaume bila shaka hawataonekana katika foleni ya kuchukua fomu za kuomba
kugombea Urais. Sio hawawezi bali wameshajishusha zaidi ya walivyoshushwa wanawake
wa zama zilizopita.
Mpaka sasa historia ya Tanzania imemuandika Anna Claudia
Senkoro akiwa mwanamama pekee aliyethubutu kutaka kuchukua nguvu (power) mbele
ya wanaume tisa waliokuwa wakigombea
nafasi ya Urais. Inawezekana kabisa waliompinga na pengine kumbeza asilimia
kubwa kama sio yote ni wanawake wenzake. Wenyewe hawapendani na hawaaminiani.
Kama wanawake nchini
hawajaamua kuachana na woga unaowapelekea kutojiamini wataendeleza kuusimika
mfumo kandamizi dhidi yao kutokana na ukweli kuwa wenyewe wanaufurahia nakuukumbatia.
Ifike wakati wanawake waachwe wasimame kwa nguvu zao wenyewe na sio
kupendelewa.
0 maoni:
Chapisha Maoni
Click to see the code!
To insert emoticon you must added at least one space before the code.